Twiga Stars wapo tayari dhidi ya She-Polopolo - ALEX MWENDATZ

Breaking

Monday, April 2, 2018

Twiga Stars wapo tayari dhidi ya She-Polopolo



Kocha msaidizi wa timu ya soka ya Taifa kwa upande wa wanawake (Twiga Stars) Edna Lema ameeleza kuwa watakuwa na kibarua kizito watakapocheza na Zambia (She Polopolo) katika mchezo wa raundi ya kwanza kuwania kushiriki Kombe la Mataifa Afrika (AWCON).

Edna amesema wanatambua walipocheza nao awali kwa takribani miaka mitatu iliyopita watakuwa wamebadilika sana na watakuwa wamekomaa, lakini hata wao wanajiona wakiwa wameimarika tofauti na awali.

"Zambia ni timu ngumu, tulicheza nayo tukaifunga lakini kwa sasa wamebadilika sana, tutahakikisha tunakuwa makini ili tupate ushindi na kusonga mbele," amesema Edna.

Rekodi zao

Kwa siku za hivi karibuni timu hizo zimekutana mara mbili katika michezo ya kufuzu kwa michuano ya All Africans Games mwaka 2015 na Tanzania kuwashinda Zambia kwa jumla ya mabao 6-5, ikiwa ni kisasi kwa Twiga Stars baada ya mwaka 2014 kutolewa na Zambia kwa jumla ya mabao 3-2 katika michuano ya kufuzu kwa fainali za Afrika.

Twiga Stars itacheza dhidi ya Zambia (She Polopolo) Aprili 4, 2018 uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam na marudiano kufanyika April 8, 2018 jijini Lusaka nchini Zambia.

Mshindi wa jumla kwa raundi hii atacheza na mshindi kati ya Namibia na Zimbabwe mwezi Mei, na atakayeibuka mshindi atafuzu moja kwa moja kwa Fainali hizo wa Wanawake Afrika, ambazo zitafanyika nchini Ghana mwaka huu.

No comments:

Post a Comment