SINGIDA UNITED NA MTIBWA SUGAR BONGE LA MECHI NAMFUA LEO - ALEX MWENDATZ

Breaking

Friday, April 6, 2018

SINGIDA UNITED NA MTIBWA SUGAR BONGE LA MECHI NAMFUA LEO


SINGIDA United wanawakaribisha Mtibwa Sugar katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Namfua leo utakaoonyeshwa moja kwa moja na Azam Sports 2 kuanzia Saa 10:00 jioni.

Singida United ya kocha Mholanzi, Hans van der Pluijm inaingia kwenye mchezo wa leo ikiwa na kumbukumbu nzuri baada ya kuitoa Yanga SC katika Robo Fainali ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) kwa penalti 4-2 baada ya sare ya 1-1 Jumapili.
Kama Mtibwa Sugar tu, nayo Jumamosi iliitupa nje Azam FC kwa penalti 9-8  baada ya sare ya 0-0 katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.


Katika Nusu Fainali, wakati Singida United itamenyana na JKT Tanzania, Mtibwa Sugar watamenyana na Stand United mechi hizo zikichezwa kati ya Aprili 16 na 18, mwaka huu.
Katika Ligi Kuu timu hizo zinafuatana kwenye nafasi ya tano na sita, Singida United iliyopanda msimu huu ikiwa juu kwa pointi zake 36 baada ya kucheza mechi 22 na Mtibwa Sugar wakiwa na pointi 27 za mechi 20.      

Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo ni kati ya Mbao FC na Lipuli FC ya Iringa Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, ambayo itaanza Saa 10:00 jioni na kuonyeshwa na Azam Sports HD.
Mbao FC ni moja ya timu zilizo hatarini kushuka daraja, ikiwa nafasi ya 14 katika ligi ya timu 16 kwa pointi zake 19 za mechi 22, mbele ya Njombe Mji FC yenye pointi 18 za mechi 22 na Maji Maji FC pointi 16 za mechi 22.

Lipuli FC inayofundishwa na wachezaji wa zamani wa Simba SC, Suleiman Matola na Amri Said ina pointi 27 za mechi 22 katika nafasi ya saba, juu ya Mbeya City na Ruvu Shooting ya Pwani zenye pointi 25 kila moja baada ya kucheza mechi 22 pia. 

No comments:

Post a Comment